Na: Gerald Lwomile
Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imesema itahakikisha shule zote zenye mchepuo wa Kilimo nchini kuhakikisha zinakuwa na uwezo wa kuzalisha mazao ya chakula kwani hiyo ndiyo njia sahihi ya kufahamu kilimo na namna kinavyofanyika.
Akizungumza na wanafunzi na waalimu wa Shule ya Sekondari ya Kilimo iliyoko Kilosa Mkoani Morogoro Novemba Mosi, 2019 Waziri Profesa Ndalichako amesema Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dkt John Pombe Magufuli inataka kuhakikisha hakuna uhaba wa chakula katika shule hizo.
Amesema awali katika shule nyingi zenye mchepuo wa kilimo hazikuwa hata na mashamba na kushangaa inawezekana vipi shule wanafunzi wanasoma mambo ya kilimo lakini hakuna hata shamba linaloonyesha kuwa kweli kuna masomo ya kilimo.
Katika hatua nyingine Waziri huyo wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, amewaonya Maafisa Elimu wa Mikoa yote hapa nchini wanaomdanganya Rais kuwa wamemaliza tatizo la upungufu wa madarasa na badala yake wanaongeza idadi ya wanafunzi katika shule na kusababisha wanafunzi hao kufanya vibaya katika matokeo ya mtihani wa mwisho.
Amesema vitendo hivyo vinasababisha walimu wa shule hizo kushindwa kufundisha kwa ufanisi na matokeo yake wanafunzi kushindwa kufanya vizuri katika masomo yao.
Akizungumzia ukarabati unaofanywa na Wizara yake katika Shule ya Sekondari ya Kilimo ya Kilosa ambayo imepewa zaidi ya shilingi milioni 750 amesema ukarabati huo ni kuigwa kwani sasa shule inamuonekana mzuri huku kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 150 kikiwa kimebaki
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Adam Mgoya amesema kuwa mafanikio ya ukarabati huo unatokana na ofisi yake kusimamia kwa karibu zaidi ili kuhakikisha fedha hizo zilizotolewa na Serikali zinatumika vizuri na kuleta tija katika elimu.