NA GLADNESS N. MPHURU
Imeelezwa kuwa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kinaongoza Kitaifa kwa kufanya tafiti na kuandika machapisho yenye tija hususani ya Sayansi za Kilimo ambayo yanawafikia walengwa wa ndani na nje ya mipaka ya Tanzania.
Hayo yamebainishwa na Mratibu wa Utafiti na Machapisho SUA, Prof. Japhet Kashaigili wakati akifungua Warsha ya siku tano inayolenga kujenga uwezo juu ya uandikaji wa machapisho chuoni hapo.
Prof. Kashaigili ameeleza malengo makuu ya Warsha hiyo kuwa ni kuwajengea uwezo Watafiti wa kujua namna ya kuziandika tafiti zao ili kuleta tija, kutafuta njia ya machapisho kumfikia mlengwa kiurahisi, kuongeza uwezo wa kutafsiri matokeo ya kisayansi kwenye lugha nyepesi na yenye kueleweka kulingana na matakwa ya jamii inayolengwa.
“Uandaaji wa machapisho hayo unahitaji utaratibu fulani na huo utaratibu mara nyingi kwa vijana ambao wametoka shule labda amemaliza PHD au wengine bado wanafanya Masters wanahitaji kujengewa uwezo ili waweze kujua namna ya kuandika machapisho ambayo yanaendana na mahitaji ya kitaaluma, mahitaji ya kijamii na ya kisera”, amesema Prof. Kashaigili
Prof. Kashaigili amesema sababu za tafiti nyingi kuishia kwenye makabati na watafiti wengi kushindwa kuandika tafiti zenye mlengo wa jamii ni kutokana na mahali ambapo chapisho limechapishwa, mvuto wa chapisho, sanjari na mchango wa chapisho husika katika kuleta maendeleo ya walengwa na nchi kiujumla.
“Tafiti zenye malengo makubwa na mapana kwa nchi zinatokana na hoja zilizopo ndani ya nchi ambazo zinahitaji utatuzi”, alisisitiza Mratibu huyo
Aidha ametoa Rai kwa watafiti wachanga kuwa wepesi katika kujifunza na kuwa na kiu ya kufikia hatua kubwa na hata hatua ya ubobezi kwenye tafiti.