Na Amina Hezron,Morogoro
Mwenyekiti wa Ndaki ya Tiba za Mifugo na Sayansi za Wanyama VET ameitaka ndaki hiyo kujitangaza kupitia vyombo vya habari ili wananchi waweze kufahamu shughuli zinazofanywa na ndaki hiyo na jamii kuweza kufaidika.
Akizungumza na SUAMEDIA leo Mwenyekiti Dr Henry Bwille amesema kuwa katika ndaki hiyo kuna mambo mengi yanayofanyika ambayo yanaweza kusaidia jamii ambayo mpaka sasa haifahamu kama mambo hayo yanafanyika SUA ndani ya ndaki hiyo.
“Yale maswala yote yanayotendeka hapa chuoni ambayo yanahusu jamii ambayo jamii inaweza kufaidika hata Tanzania nzima kwa ujumla ningeomba wajitangaze ili kuweza kufikia muafaka wa taarifa zetu zijulikane hata wakipata shida waweze kutukimbilia,nimeona kuna dawa za mitishamba zimetengenezwa zinatibu vidonda vya tumbo, vidonda sugu hadi kisukari cha wanyama lakini nnje watu hawajui wanajua wao wenyewe tu”, alisema Dr Bwille.
Aidha Mjumbe wa Bodi ya ndaki hiyo ambae muwakilishi wa wajumbe wengine wa bodi Dr Abdu Hayghaimo amemshukulu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Prof Raphael Chibunda kwakuwawezesha kutembelea sehemu mbalimbali za ndaki hiyo ambazo zinatoa mafunzo kwa wanafunzi ambao wanakwenda katika tiba za udaktari pamoja na tiba zingine lakini pia na kuwanufaisha wakulima wanaozunguka eneo la chuo.
Pia amewaomba kuzingatia yale walioelezwa na mwenyekiti wa bodi hiyo kwakuwa ndaki hiyo inahuduma nzuri na uwezo mkubwa wa kutambua chanzo na sababu za magonjwa kitu ambacho wananchi hawakifahamu hivyo wajitahidi kujitangaza ili wananchi waweze kufaidi huduma zitolewazo hapo.
Kwa upande wake Rasi wa ndaki ya Tiba za Mifugo na Sayansi za Wanyama Prof Amandus Muhairwa amepokea vizuri mawazo yaliyotolewa na mwenyekiti wa bodi na ameahidi kuyafanyia kazi kwa haraka ili mambo yaweze kwenda kama ilivyopendekezwa.
“swala la kujitangaza na kuifanya ndaki yetu ieleweke kwa wadau hiyo ametupatia changamoto kubwa ambayo tunakwenda kuifanyia kazi, ni kweli tunafanya mambo mengi lakini ni wazi kwamba hayajulikani kiasi ambacho inapaswa katika jamii yetu”, alisema Prof Muhairwa.