Na: Josephine Mallango
Wakati dunia ikishuhudia kuendelea kuenea kwa maambukizi ya Virusi vya Corona, Daktari Mkazi wa SUA Omar Kasuwi ametoa wito kwa wanajumuiya wa SUA na watanzania kulazimika kujifunza kubadili tabia na kuacha mazoea hasa katika masuala yanayogharimu maisha ya watu.
Akizungumza katika kipindi cha Mchakamchaka SUA Radio leo Marchi 24, 2020 , Dkt. Kasuwi amesema ugonjwa huo unaotokana na virusi vya Corona (Covid-19) unaua na mpaka sasa dunia haijapata dawa wala chanjo ya virusi hivyo tangu kugundulika kwake nchini China Disemba 2019.
Ameongeza kuwa suluhisho la kuepukana na kuenea kwa maambukizi ya virusi hivyo ni kuchukua tahadhari na kufuata miongozo inayotolewa na wataalam kwa kuzingatia kanuni na misingi ya afya nyakati zote
Akizungumzia tahadhari katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA amesema chuo kilianza kuchukua tahadhari mapema kabla ya kuingia kwa virus hivyo nchini ikiwa ni pamoja na kuundwa kwa Kamati ya Kushauri Chuo juu ya virusi vya corona ,uhamasishaji katika kunawa mikono kwa kutumia maji na sabuni au vieuzi ‘sanitizer’ kwa watumishi wawapo ofisini na majumbani pamoja na maboresho katika Hospitali ya SUA ikiwemo kutoa elimu kwa wahudumu wa Afya .
Dkt. Kasuwi amebainisha kuwa virusi vya corona vinaambukiza kwa njia mbili ambazo ni uambukizaji wa moja kwa moja na uambukizaji usio wa moja kwa moja na kwamba ndio maana inahimizwa kuchukua tahadhari ya kwanza kwa kunawa mikono kwa muda wa sek 20, matumizi ya barakoa pale ambapo mgonjwa anaona anaweza kuambukiza wengine pamoja na vieuzi mara kwa mara.
KATIKA VIDEO BOFYA HAPA CHINI