Na Gerald Lwomile
Imeelezwa kuwa pamoja na kuwepo vyanzo vingi vya ufugaji wa Samaki nchini lakini bado havijatumika ipasavyo jambo linalosababisha kuwepo kwa upungufu mkubwa wa kitoweo hicho katika soko
Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu ya Kujiendeleza ICE – SUA Dkt. Devotha Kilave aliyesimama katikakati amevaa kitenge akiwa na Mkufunzi wa Mafunzo ya ufugaji wa Samaki Dkt. Hieromin Lamtane kulia aliyefaa shati la kijani mpauko, Mratibu wa mafunzo hayo Dkt Innocent Babili aliyevaa miwani kushoto na washiriki wa mafunzo hayo ( Picha na Gerald Lwomile)
Akizungumza katika mafunzo ya ufugaji wa Samaki aina ya Kambale yaliyoanza leo Disemba 16, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Mkufunzi katika mafunzo hayo Dkt. Hieromin Lamtane amesema soko la Samaki nchini ni kubwa ukilinganisha na wanaozalishwa
Amesema upatikanaji wa Samaki umekuwa mgumu na idadi ya Samaki inapungua kutokana na ongezeko la watu, mabadiliko ya tabianchi, uharibifu wa mazingira na nguvu kubwa ya uvuvi inayotumika iki ni pamoja na uvuvi haramu
Dkt. Lamtane akitoa mafunzo ya ufugaji wa samaki aina ya Kambale katika mafunzo yanayofanyika SUA ( Picha na Gerald Lwomile)
Dkt. Lantane amesema kuwa pamoja na kuwepo kwa wasiwasi kwa baadhi ya wafugaji kuwa hakuna soko zuri la Samaki lakini ukweli ni kuwa Samaki wana soko kubwa nchini na ni muhimu mfugaji kujua ni Samaki gani anafuga na awafuge katika ukubwa gani kulingana na soko analokwenda kuwauza
“ kwa hiyo lengo kuu la ufugaji wa Samaki ni kujipatia kipato na chakula zamani watu walifuga kwaajili ya chakula lakini mahubiri ya sasa ni biashara, tunahitaji kipato, lakini pia ni ajira na pia tunapata lishe” amesema Dkt. Lantane
Naye mfugaji wa Samaki na mzalishaji wa vifaranga vya Samaki Bibi Rehema Mwaluka wa Mkoa wa Pwani amesema katika ufugaji wa Samaki wamekuwa wakibaliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na uzalishaji kuwa duni, usafi na hata gharama za chakula
” Kwa upande wa uzalishaji ukikosea kidogo vifaranka vinakuwa havistawi vizuri, jambo la pili uangilizi wake katika usafi ukiviacha namakapi yatokanayo nakuanguliwa inakuwa changamoto maana yanatengeneza fangasi na pia wenyewe kwa kulana na upatikanaji wa chakula cha Samaki” amesema Bibi Mwaluka
Kwa upande wake Bw. Steven Mrashani wa Morogoro amesema tangu ameanza kufuga Samaki aina ya kambale hajakutana na changamoto kubwa kama alipokuwa akifuga Samaki aina ya Sato na kuwataka wafugaji nchi kuingia katika ufugaji ili kujiletea maendeleo
” Tangu nimeanza kufuga Kambale sijakutana na changamoto nyingi kama ilivyokuwa kwa sato, tatizo ni suala la ukuaji ndilo linaloenda polepole sana na nitarajia kupata mafunzo haya basi nitatatua changamoto hiyo” amesema Mrashani
Awali akifungua mafunzo Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu ya Kujiendeleza ICE SUA Dkt. Devotha Kilave amesema SUA kupitia ICE itaendelea kuhakikisha inawasaidia wanachi kwa kuwafikishia taarifa mbalimbali ikiwa ni pamoja na tafiti, ubunifu na teknolojia mbalimbali zinazozalishwa chuoni hapo
Mafunzo hayo yamewashrikisha zaidi ya washiriki 20 wakiwemo wakuu wa Idara za Uvuvi, wafugaji wazoefu na wale wanaojifunza kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania