Na Gerald Lwomile
SUA
Makamu wa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Prof.Raphael Chibunda amesema SUA itahakikisha inakabiliana na tatizo la nchi kuwa na mifugo duni ili kuwa na mifugo bora na kumsaidia mfugaji wa Tanzania kuzalisha mifugo itakayomletea tija
Makamu wa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Prof. Chibunda akikata utepe kuashiria uzinduzi wa mtambo huo kushoto ni Kaimu Rasi wa Ndaki ya Tiba ya Wanyama na Sayansi za Afya Prof. Muhairwa na kulia ni aliyekuwa kiongozi wa Mradi wa TALI Prof. Kazwala ( Picha na Gerald Lwomile)
Kauli hiyo ameitoa leo Januari 10, 2019 wakati SUA ikikabidhiwa mtambo wa uhamilishaji yaani upandikizaji wa mbegu kwa wanyama mtambo uliokuwa ukitumiwa na Mradi wa Afya ya Wanyama na uboreshaji wa makazi “HALI” makabidhiao yaliyofanyika katika Ndaki ya Tiba ya Mifugo na Sayansi za Afya
Prof. Chibunda amesema Serikali ambayo inaongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli na kwa kauli yake amekuwa akitaka nchi hii iwe na uzalishaji hivyo ni muhimu SUA ikahakikisha inawawesha wakulima kuzalisha kwa tija na kuleta maendeleo nchini
“Ukiangalia wito anaoutoa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli ni kuisukuma hii nchi ili iweze kuzalisha kwa tija kwa kila sekta na tija katika uzalishaji wa mifugo kwa kweli bado iko chini na mojawapo la tatizo kubwa la nchi hii ni uzalishaji duni wa wanyama ambao ni bora, sasa uwepo wa huu mtamba hapa sisi kama chuo lakini pia kama watanzania utatupa uwezo wa kutafuta ng’ombe ambao ni bora Zaidi” amesema Prof. Chibunda
Makamu wa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Prof. Chibunda akiwasha mtambo na kuzalisha hewa ya Nitrojeni kushoto ni Kaimu Rasi wa Ndaki ya Tiba ya Wanyama na Sayansi za Afya Prof. Muhairwa na kulia ni aliyekuwa kiongozi wa Mradi wa TALI Prof. Kazwala ( Picha na Gerald Lwomile)
Awali akimweleza namna mtambo huo unavyofanyakazi aliyekuwa Mkuu wa Mradi wa HALI na Mkufunzi Mwandamizi katika Ndaki ya Tiba ya Wanyama na Sayansi za Jamii Prof. Ludovick Kazwala amesema mtambo huo ni wa kisasa na utasaidia Chuo na watanzania kwa ujumla
Naye Afisa Mifugo wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Gasper Msimbe amesema mtambo huo wa kuzalisha gesi ya Nitrogeni uliozinduliwa SUA utasaidia wafugaji wengi na kupunguza gharama kwani awali mkoa ulilazimika kuagiza gesi hiyo nje ya mkoa
“Lakini sasa hivi kwa sababu gesi inazalishwa hapa mkoani Morogoro katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo itarahisisha suala la uhimilishaji katika mkoa wa Morogoro halitakuwa tatizo tena” amesema Msimba
Akizungumzia namna mtambo huo utakavyofanyakazi mtaalamu kutoka Idara ya Uhimilishaji na Uzalishaji kutoka SUA Dkt. Isaac Kashoma amesema njia ya uhamilishaji huja na wanyama bora kwani mbegu huchaguliwa kutoka mnyama bora na mchakato hupitia maabara
Prof. Kazwala kulia akitoa maelezokwa Makamu wa Mkuu wa Chuo Prof. Chibunda katikati aliyevaa miwani jinsi mtambo huo unavyofanya kazi (Picha na Gerald Lwomile)
“Mtambo huo wa kuzalisha Nitrojeni una uwezo wa kuzalisha lita 200 kwa wiki na ukiangalia zoezi la uhamilishaji lita 35 ziunaweza kutunzwa na mtaalamu kwa miezi miwili kwa hiyo tuna uwezo wa kutunza mitungi 3 kwa wiki moja ambayo inauwezo wa kutosheleza wila 3 za watu wanaofanya uhamilishaji” amesema Kashoma